Thursday 4 December 2014

MGOGORO WA MPAKA KATI YA TANZANIA NA MALAWI..HALI BADO NI TETE



Kile kilichoonekana kuanza kama mzaha kati ya Tanzania na Malawi kuhusu umiliki wa Ziwa Nyasa, sasa kimeanza kuchukua sura mpya kwa kila nchi kuendelea kutekeleza kitu inachokiamini kuwa ni sahihi.

Baada ya kutokea vuta nikuvute kati ya nchi hizo mbili zilizokuwa marafiki wa miaka mingi, marais wastaafu kutoka Msumbiji, Joaquim Chissano, Festus Mogae wa Bostwana na Thabo Mbeki wa Afrika Kusini walipewa jukumu la kutafuta maridhiano.

Hivi karibuni marais hao walikutana na Rais Peter Mutharika kwa ajili ya kuzungumzia jambo hilo, lakini kwa bahati mbaya walichodhani kuwa ni jambo dogo, kiligeuka kuwa ‘mfupa mgumu’ baada ya rais huyo kusema Tanzania haimiliki hata inchi moja ya Ziwa Nyasa.

Kama hiyo haitoshi, Mutharika anasema kuwa msimamo wake hauwezi kubadilika kwa kuwa mipaka ya nchi hizo mbili iliwekwa na wakoloni na kuipa uhalali Malawi umiliki wa ziwa hilo.

Wakati hayo yakiendelea huko Malawi, hapa nchini Serikali inaendelea na mipango ya kuboresha miundombinu ndani ya ziwa hilo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa meli yenye uwezo wa kubeba abiria 200 na mizigo tani 200.

Pia Serikali imeanza maandalizi ya kuweka umeme kwenye Bandari ya Kyela, unaofadhiliwa na Wakala wa Umeme Vijijini (Rea).

Alipotembelea maendeleo ya miradi hiyo hivi karibuni, kiongozi wa timu ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Florence Mwanri alisema miradi hiyo itakapokamilika itahudumia wananchi wa Mbeya, mikoa ya jirani na nchi za Malawi, Zambia na Msumbiji.

Hata hivyo, kwa mujibu wa Gazeti la Nyasa Times la Malawi, wananchi wa nchi hiyo wanatofautiana kuhusu msimamo wa Rais Mutharika kuwa Tanzania inalitumia ziwa hilo kinyume na sheria ya kikoloni iliyoweka mipaka.

Baadhi ya raia wa nchi hiyo wanamwona rais wao kama shujaa anayetetea hadharani maliasili za nchi yao, huku wengine wakiutazama msimamo wa Mutharika kama ni njia ya kuvuruga uhusiano wa kibiashara baina ya nchi hizo.

“Rais Mutharika ameongea sahihi, kwa sababu sheria zilizotumika kugawa mikapa ni za wakati wa ukoloni. Kinachotakiwa kwa Tanzania ni kutambua ukweli huo,” anasema Antipas Massawe.

Mwananchi huyo anaongeza kuwa: “Tanzania na Malawi haziwezi kutatua mgogoro huo kwa sababu wao siyo waliouleta.”

Zabweka Mambo anampongeza Rais Mutharika kwa msimamo wake, huku akiwaambia wananchi kuwa mvutano huo unatokana na Tanzania kutaka kuchimba mafuta kwenye Ziwa Nyasa.

No comments: