Saturday 20 December 2014

AMISI TAMBWE AMWAGA MACHOZI HADHARANI BAADA YA KUONA NYUMBA ANAYOISHI MBUYU TWITE...

SIKU chache baada ya aliyekuwa mshambuliaji wa Simba, Mrundi, Amissi Tambwe, ajiunge na Yanga, amejikuta akitokwa na machozi baada ya kutembelea nyumbani kwa beki wa timu hiyo ambaye ni raia wa Rwanda na mwenye asili ya DR Congo, Mbuyu Twite.
Tambwe alikumbwa na hali hiyo bila ya kutegemea kutokana na kujionea maisha mazuri ambayo anaishi beki huyo huku akiambiwa kuwa na wachezaji wengine wa timu hiyo nao wanaishi vizuri kama ‘professional’. 


Ndugu wa karibu wa Tambwe, ameliambia Championi Jumamosi kuwa hali hiyo imefanya Tambwe ajione kama mtu aliyekuwa amepotea lakini mwisho wa siku anaamini kuwa hivi sasa naye ataishi maisha mazuri kama wachezaji wenzake wa kimataifa wa Yanga.
“Maisha aliyokuwa akiishi Simba siyo kama ya mchezaji wa kulipwa, yalikuwa ya kawaida sana ila kwa sasa kutokana na utamaduni wa Yanga wa kuwajali wachezaji wake ataishi kwa amani na atafanya kazi yake kwa moyo mmoja.
“Alipokuwa Simba alikuwa akiishi kama yupo jeshini, nyumba moja watu kibao ukikaa vibaya vitu vyako unaibiwa lakini sasa anaamini ataishi kwa amani kabisa,” alisema mtoa habari huyo na kuongeza: 
“Watu wengi najua hawataamini juu ya hili lakini ukweli ndiyo huo, Yanga inawajali sana wachezaji wake ukilinganisha na Simba na kama hawaamini basi watembelee sehemu ambazo wachezaji hao wanaishi na watapata jibu.”
Tambwe amejiunga na Yanga kwa mkataba wa mwaka mmoja ambao utamwezesha kujikusanyia jumla ya Sh milioni 78. Milioni 34 zinatokana na usajili wake na zilizobakia zinatokana na mshahara wake atakaokuwa akilipwa kwa mwezi.


No comments: