Tuesday 9 December 2014

ALIYEZAMISHWA SULULU KICHWANI APONA KABISA.....


HAKUNA neno jingine la kutumia zaidi ya kusema; KWELI MUNGU MKUBWA! Ni miezi mitano sasa imekatika tangu kusambaa kwa picha mitandaoni zilizomwonesha mwanaume mmoja akiwa ameshindiliwa sululu kichwani hukukisa kikiwa hakijulikani. 


Baadhi ya mitandao iliandika kuwa, jamaa huyo apigwa sululu baada ya kufumaniwa na mke wa mtu gesti, mingine ikasema hapana, alipigwa sululu katika kugombea madini machimboni, wengine wakasema kwanza tukio lile halikuwa Tanzania. 

SASA MAMBO HADHARANI


Hivi karibuni, timu ya waandishi wa Global jijini Mwanza ilimchimba mwanaume huyo mpaka ikampata na kubaini kwamba anaitwa Oka Kaombe. 
Oka ni mkazi wa Mtaa wa Nyakazuzu, Kata ya Nyamatogo wilayani Sengerema, Mwanza ambapo waandishi wetu walimtembelea nyumbani anakoishi na baba yake mzazi (mzee Kaombe) na kuzungumza naye ‘ei tu zedi’ kuhusu mkasa wake huo wa kuzamishwa sululu kichwani. 


Kovu la sululu kama linavyoonekana kichwani mwa Bw. Oka Kaombe.

KUZAMISHWA SULULU 
KICHWANI 
“Kwanza kabisa napenda kusema kweli Mungu ni mkubwa, nimepona! Ingawa mwili bado hauna nguvu sawasawa lakini naendelea vizuri. “Ilikuwa tarehe 19, Julai mwaka 2013 katika machimbo ya Mgodi wa Miombo- Rwamgasa wilayani Geita, mimi ni fundi wa kuchimba maduara yanayotumika kuchimbia dhahabu. 

“Baada ya kumaliza kazi zangu majira ya jioni, nikaenda kupumzika ili kujiandaa kwa siku iliyofuata. “Nilikuwa nimepumzika na wenzangu zaidi ya mia moja, unajua tena migodini. Kufika saa 3 hivi usiku nikiwa nimeanza kusinziasinzia, nilishtukia kitu kizito kinaingia kichwani mwangu upande wa kushoto.”

ALISHINDWA KUPIGA KELELE
“Nilishindwa kupiga kelele nadhani kwa sababu ya kule kusinzia. Wenzangu ambao nao walianza kulala walishtuka kwa kusikia harufu ya damu, wakaamka na kuja wakanikuta sululu ikiwa imezama kichwani. 


Nilianza kujitambua baada ya siku nne nikiwa palepale Bugando na kujikuta nipo hospitali lakini nilikuwa siwezi kuzungumza wala kusikia vizuri. Maumivu yalikuwa makali sana kutokana na sululu kuzama kichwani maana ilipoingia ilikwenda kutokea upande wa pili wa kichwa. “Nikiwa nimeshafanyiwa upasuaji kwa kuchomolewa sululu, niliendelea kukaa Bugando kwa siku 52.” 

ATOROKA BUGANDO, AMSAKA MBAYA WAKE
Oka alisema kuwa, hiyo siku ya 52 aliamua kutoroka hospitalini hapo kwa sababu alishindwa kulipia gharama za matibabu ambazo ni shilingi laki tisa (900,000). “Kiasi hicho cha pesa kwangu kilikuwa kikubwa na hata sasa bado ni kikubwa ndiyo maana niliamua kutoroka,’’ alisema Oka.

ALIYEMZAMISHA SULULU AJULIKANA
Oka anaendelea kusimulia:Sululu iliyotolewa kichwani mwa Bw. Oka Kaombe 

“Nilipotoka hospitalini kitu cha kwanza nilianza kumtafuta mtu aliyenifanyia kitendo kile cha kinyama, marafiki zangu wakanipa ushirikiano na kuniambia unyama ule ulifanywa na jamaa mmoja anayeitwa Masha. “Huyu Masha ni mchimbaji wa madini kwenye ule mgodi lakini alikimbia baada ya kufanya tukio na mpaka sasa hajulikani alipo.”

KISA CHA KUPIGWA SULULU PIA CHAJULIKANA

Oka alisema taarifa alizopata baadaye kutoka kwa wachimbaji mgodini hapo ni kwamba, lengo la Masha kumpiga na sululu lilikuwa ni kumtoa kafara (ndagu) ili aweze kupata dhahabu nyingi na awe bilionea kwa siku za usoni. “Ila Mungu ni mkubwa alitupilia mbali wazo hilo mpaka sasa niko hai,” alisema Oka. 

AFYA YAKE KWA SASA
Oka alisema kwa sasa anaamini amepona kabisa kidonda chake kichwani ila hawezi kufanya kazi yoyote kutokana na mwili kukosa nguvu za kutosha. 

UPASUAJI MWINGINE
Aliendelea kusema kuwa, akiwa Bugando aliambiwa na madaktari kuwa anatakiwa kufanyiwa upasuaji kwa mara nyingine na kuwekewa vyuma kichwani baada ya kuwekewa vyuma hivyo itabidi akae miaka mitatu bila kufanya kazi yoyote ndipo atapata nguvu za kufanya kazi kama zamani. 


MAISHA YAKE KWA SASA
Oka alisema maisha yake kwa sasa ni magumu kwani ana watoto 5, lakini pia alitengana na mke wake hivyo yeye ndiye baba na mama wa familia kwani hata wazazi wake wamezeeka, hivyo wanamtegemea yeye.

ANACHOWAOMBA WATANZANIA
Alisema kwa sababu bado ana safari ya kujitibu na pia kutunza familia, amewaomba Watanzania wenye kuguswa na mkasa wake wamsaidie pesa kwa kiasi chochote atakachojaliwa mtu kwa kutumia simu yake ya mkononi ambayo ni 0682 013479.
CHANZI:GPL

No comments: