Thursday 27 November 2014

UBAGUZI WA RANGI WAKITA MIZIZI MAREKANI....WATU WEUSI WAWEKWA GEREZANI,WAHUKUMIWA KIFO NA WENGINE WAPIGWA RISASI NA POLISI


Mkuu wa Haki za Binaadamu Katika Umoja wa Mataifa ameelezea wasiwasi wake kuhusu 'ubaguzi uliokita mizizi' na idadi kubwa kupita kiasi ya Wamarekani weusi au wenye asili ya Afrika ambao wanauawa na polisi nchini Marekani.

Zeid Ra’ad Al Hussein Kamishna wa Haki za Binadamu katika Umoja wa Mataifa ameongeza kuwa kuna idadi kubwa kupita kiasi ya Wamarekani weusi wanaoshikiliwa gerezani na wanaosubiri kutekelezwa hukumu za kifo dhidi yao.

Matamshi hayo yametolewa kufuatia ghasia kubwa zilizoibuka baada ya jopo la mahakama huko Missouri, Marekani kumuondoa hatiani afisa mzungu wa kikosi cha polisi ambaye alimpiga risasi na kumuua kijana Mmarekani mwenye asili ya Afrika, Michael Brown, katika mji wa Ferguson. Ghasia zimeripotiwa katika miji zaidi ya 90 kote Marekani ambapo waandamanaji wanalalamikia ukandamizaji na ubaguzi wa wazi dhidi ya watu wenye asili ya Afrika katika mfumo wa utawala nchini Marekani. Gavana wa Jimbo la Missouri, Jay Nixon, ameagiza wanajeshi wengine 2,200 wa Gadi ya Taifa kupelekwa Ferguson kukabiliana na waandamanaji wenye hasira.

No comments: