Saturday 17 January 2015

WATUHUMIWA WENGINE 3 WA SAKATA LA ESCROW WAFIKISHWA MAHAKAMANI

Maafisa watatu mmoja wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Mamlaka ya Mapato (TRA) pamoja na wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) leo wamefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuhusiana na  kashfa ya akaunti ya Tegeta Escrow.

Waliofikishwa katika mahakama hiyo leo jijini Dar es Salaam, ni Mwanasheria wa TANESCO Stephen Urassa, Afisa Misamaha ya Kodi (TRA) Kyabukoba Mutabingwa na Mkurugenzi wa Fedha (BOT) Julius Angelo ambao wote wanatuhumiwa kuchukua rushwa ya fedha za akaunti ya Escrow.
  
Katika kesi hiyo iliyoletwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Urassa anashtakiwa kwa kuchukua rushwa ya shilingi milioni 161.7, Angelo anashtakiwa kuchukua rushwa ya shilingi milioni 161.7 na Mutabingwa kwa kupokea shilingi bilioni 1.6.
  
Mtuhumiwa Stephen Urassa ametoka nje kwa dhamana wakati wenzake Kyabukoba Mutabingwa na Julius Angelo wamepelekwa rumande baada ya kushindwa masharti ya dhamana.


No comments: