Tuesday 25 November 2014

NAMBA ZOTE ZA SIMU KUSAJILIWA UPYAAAAAAAAAAAAA


SERIKALI imesema itafanya tena usajili wa namba zote za simu za mkononi nchini ili kuthibitisha zinazotumika.

Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba alisema hayo bungeni jana wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge kupitia Baraza la Wawakilishi, Jaku Hashim Ayoub (CCM).

January alikiri ni kweli kuwa wapo watu wanaotumia majina feki katika kusajili namba zao za simu za mkononi, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

“Wapo watu wanaotumia majina na vitambulisho feki wanaposajili namba zao. “Tunaomba waheshimiwa wabunge mtuunge mkono tutakapotangaza usajili mpya wa namba za simu,” alisema Naibu Waziri January.

Aidha, alisema Serikali inakusudia mwakani kuwasilisha muswada wa kutunga sheria tatu ili kudhibiti usalama katika mitandao ya mawasiliano.

Akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema), Naibu Waziri alikiri kuwapo kwa utapeli kwa kutumia mitandao ya intaneti, pia akakiri uwezo mdogo wa vyombo vya ulinzi na usalama katika kuchunguza, kubaini na kudhibiti matumizi hayo.

Alisema sheria zinazopendekezwa zitadhibiti hali hiyo. Katika swali lake la nyongeza, Mdee alisema kumekuwapo na uhalifu wa kutumia mitandao ya intaneti na kuwataja waliowahi kuhusishwa katika utapeli huo kuwa ni yeye mwenyewe, wabunge Kabwe Zitto na Edward Lowassa na Kampuni ya IPP.

Akijibu swali la msingi la Ayoub, Naibu Waziri January alisema kwa mujibu wa sheria, ni kosa la jinai kutumia au kuwezesha kutumika Sim Card isiyosajiliwa. Alisema atakayebainika anatumia atapewa adhabu ya faini ya Sh 500,000 au kifungo cha miezi mitatu jela.

Pia muuzaji yeyote atakayebainika kuuza Sim Card ambazo hazijasajiliwa atakuwa ametenda kosa la jinai, na atalipa faini ya Sh milioni tatu au kifungo cha miezi 12 au adhabu zote zinaweza kutekelezwa kwa pamoja.

MAKINDA AWA MBOGO SAKATA LA ESCROW


SPIKA wa Bunge, Anne Makinda amerejea bungeni kwa kishindo, baada ya jana kukataa pendekezo la kusitisha kazi nyingine za Bunge kujadili taarifa ya kukamatwa kwa baadhi ya watu wanaodaiwa kusambaza ripoti kuhusu akaunti ya Tegeta Escrow ya IPTL.

Aidha, amesema wabunge watamuonesha ni kwa jinsi gani amehongwa Sh bilioni 1.6 (Dola za Marekani milioni moja) katika sakata hilo.

Akiongoza Bunge kwa mara ya kwanza katika Mkutano wa 16 na 17 baada ya kuwa safarini kwa muda mrefu, Makinda pia ameahidi kuwa wabunge watapewa ripoti hiyo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kuhusu sakata la fedha za IPTL.

Alitoa maelekezo hayo baada ya Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia (NCCR-Mageuzi), kuomba kupitia Kanuni za Bunge, shughuli za Bunge zilizopangwa zisiendelee badala yake wabunge wajadili kusambazwa kwa nyaraka za CAG zinazodaiwa kuibwa ofisini kwa Spika.

Mbatia alisema kumekuwapo na taarifa za mtu kudurufu ripoti hiyo na kuisambaza kwa wabunge na watu mbalimbali, jambo ambalo ni kinyume cha Kanuni.

Hivyo, kwa kutumia Kanuni za Bunge, alitaka Spika asitishe shughuli nyingine na jambo hilo lijadiliwe.

“Kazi ya Bunge ni kuisimamia Serikali, sasa hili linashusha hadhi ya Bunge isifanye kazi yake vizuri, kwa hiyo napendekeza tulijadili hapa. Naomba mambo mengine yasitishwe, tulijadili,” alisema Mbatia.

Lakini Makinda licha ya kumpongeza Mbatia kwa kulieleza hilo, alithibitisha kuwa Polisi wanamshikilia mtu mmoja kuhusu suala hilo, lakini akawahoji wabunge kwamba sasa wanataka kujadili nini.

“Sasa mnataka tujadili nini? Hatuendeshi Bunge bila taratibu. Mmeandika ninyi hizo nyaraka? Ofisi yangu imedhalilishwa. Lakini hili tayari liko Polisi, linashughulikiwa na wenzetu hawa. “Watamhoji huyo mtu alipata wapi nyaraka hizo na kuna mahali walipochapia Dar es Salaam wataenda ku-confiscated (kutaifisha). Kwa hiyo, hapa hakuna la kujadili, labda wangekuwa wamemaliza kazi yao ya uchunguzi,” alisema Makinda huku baadhi ya wabunge wakiendelea kumbana.

Mbunge wa Mkanyageni, Habib Mohamed Mnyaa (CUF), alipopewa fursa ya kuzungumza , alidai kuwa suala hilo ni vyema likajadiliwa kwani kuna nyaraka zaidi zinawekwa katika makazi ya wabunge na usalama wao uko hatarini.

Mnyaa alikwenda mbali zaidi na kumweleza Spika kuwa “ipo minong’ono pia inakuhusisha nawe Spika kwamba umehongwa Dola za Marekani milioni moja. Sasa ni bora tukajadili suala hilo,” alisema Mnyaa.

Ni kama alikuwa amemtonesha zaidi Spika Makinda, kwani alikuja juu na kusema: “Mtanionesha, mtanionesha, mtanionesha hizo hela. Hatuwezi kufanya mambo ya kitoto.”

Akimjibu Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu, Makinda alisema ni vyema wote wenye nyaraka hizo wakazirudishe Polisi.

Akijibu ombi la Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka (CCM) la kutaka ripoti hiyo ya CAG na vielelezo vyake kupewa wabunge mapema ili kujiandaa na mjadala, Spika alisema utaratibu unaandaliwa.

Akichangia mjadala wa Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2014, Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema), alisema mtu aliyekamatwa akisambaza nyaraka hizo ana uhusiano wa karibu na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.

Alisema kuwa polisi wanataka kumpeleka mtuhumiwa huyo mahakamani ili baadaye Bunge lizuiwe kujadili suala lake kwa kuwa litakuwa limefikishwa katika mhimili huo mwingine wa Dola, hivyo kikanuni watazuiwa kulizungumzia bungeni.

Ripoti ya CAG ilikabidhiwa bungeni na Serikali, Novemba 14, mwaka huu na kisha Bunge iliikabidhi kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) siku tatu baadaye, kwa ajili ya uchambuzi na maoni kabla ya kuwasilishwa ndani ya Bunge.

Kamati hiyo ya PAC inaendelea na vikao vyake na kwa mujibu wa ratiba ya Bunge, mjadala wa ripoti hiyo utaanza kesho na unatarajiwa kuendelea kabla ya Bunge kuahirishwa Ijumaa wiki hii.

Akaunti hiyo ilifunguliwa katika Benki Kuu yaTanzania (BoT) baada ya kuwapo kwa mgogoro wa kibiashara wa Tanesco na IPTL, kampuni inayofua umeme yenye mitambo yake Tegeta, Dar

HOUSEGIRL KATILI KUPANDISHWA KIZIMBANI DISEMBA 8


Polisi wamebadilisha mashtaka ya mfanyikazi wa nyumbani aliyenaswa kwa kamera akimpiga na kumtendea unyama mtoto wa mwaka mmoja na nusu, kutoka kwa kosa la kutesa na sasa anakabiliwa na kosa la jaribio la mauaji.

Video hiyo iliwaudhi watu wengi sana kwenye mitandao ya kijamii ila babake mtoto huyo alisema walisambaza video hiyo ili kuwatahadharisha wazazi wenegine.

Mfanyakazi huyo wa nyumbani Jolly Tumuhirwe, alikuwa amezuiliwa katika gereza la Luzira na mahakama ya Nakawa kwa kosa la kutesa chini ya kifungo cha 41 kwenye katiba kinachoongelea dhidi ya mateso.

Mwanamke huyo sasa anatarajiwa kufikishwa mahakamani tarehe 8 Disemba.

Hata hivyo, msemaji wa polisi Bwana Fred Enanga, amesema "shtaka dhidi ya mwanamke huyo lilibadilishwa baada ya kupitiwa mwendesha mkuu wa mashitaka.

Tumuhirwe alikubali kosa la kumpiga mtoto huyo kwa kurunzi, tuki olililonaswa kwa kamara ya CCTV. Polisi walimfanyia Tumuhirwe uchunguzi wa kiakili na kubaini kuwa ana akili timamu.

Afisaa mkuu wa polisi Fred Enaga, amewaonya waajiri kuchunguza mbinu zinazotumika kuwachagua wasichana wa kazi, kwa sababu matendo kama haya yanaweza kutokana na matatizo ya kisaikologia.

Waziri wa Jinsia, Kazi na maendeleo ya jamii Bi Mary Karooro Okurut alipongeza juhudi za wazazi wa mtoto huyo Arnella "kutokana na kitendo hicho kwa mtoto. Ingekuwa mtu mwingine angemuua mischana huyo wa kazi lakini alifuata sheria. Pia tunapeleka marekebisho katika katiba kuhusu maslai ya watoto bungeni kuimarisha sheria zinazowajali watoto," alisema waziri huyo.

Polisi wamesema kuwa nia ya shambulio hilo haijatambulika na pia msichana huyo amefanyia kazi familia hiyo kwa siku 26 pekee. Wazazi wamesema kuwa mtoto huyo ametolewa hosipitalini na hali yake ya afya inaimarika.

Kulingana na msemaji wa polisi Fred Enaga, kesi hiyo iliripotiwa na Baba ya mtoto Erick Kamanzi mnamo tarehe 13 Novemba katika kituo cha polisi cha Kiwatule baada ya kuona video hio.

Kesi hiyo ilipelekwa kwa kitengo cha polisi cha Kiira. Baada ya uchunguzi, msichana huyo wa kazi alihukumiwa na shataka la mateso katika mahakama ya Nakawa na kuzuuliwa katika gereza la Luzira.

Bwana Enaga alisema Bi Tumuhirwe alishtakiwa chini ya kifungo cha tatu kwenye katika kinacholinda maslahi ya watoto. Kifungo hicho kinajumuisha mashataka kama ya kutesa inayopeana uwezekano wa kumfunga mtu hadi miaka 15 gerezani.

Hata hivyo, Bwana Enaga anashauriana na mkurugegenzi wa pande za mashtaka kurebisha hukumu hilo kuwa kifungu cha maisha.

CASILLAS KUWANIA TUZO YA KIPA BORA DUNIANI 2014


Kipa wa Real Madrid na Uhispania Iker Casillas ameorodheshwa kwa timu ya Fifa World 2014 XI licha maonyesho yake mabaya kwenye Kombe la Dunia na kucheza michezo12 tu ligi.

Kipa wa Chelsea Thibaut Courtois yuko kwenye orodha hiyo, pamoja na Manuel Neuer wa Bayern Munich,Claudio Bravo wa Barcelona na Gianluigi Buffon wa Juventus.

Lakini kujumuishwa kwa Casillas kumeshangaza, licha yake kuwa katika timu kwa miaka mitano tangu 2008-2012.

Alicheza mechi mbili tu ya ligi ya La Liga msimu wa 2013-14 na mechi 10 zaidi msimu huu.

Mchezaji huyo mwenye umri wa 33, aliyeinua kombe la Ligi ya Mabingwa na Real, alikosa na kusababisha angalau bao moja katika mechi ya Kombe la Dunia waliocheza Uhispania dhidi ya Uholanzi na Chile, na kuwasababisha kama wamiliki kuondoka baada ya hatua ya makundi.

Courtois anaorodheshwa baada ya kuisaidia klabu ya Atletico Madrid ya Hispania kushinda ligi msimu uliopita wakati akiichezea kwa mkopo,aliendelea kuvutia akichezea Belgium katika Kombe la Dunia hadi robo fainali.

Neuer, ambaye alikuwa katika timu ya mwaka 2013, alikuwa katika lango Ujerumani ailiposhinda mashindano Brazil na pia alishinda vikombe viwili na klabu yake.

Mshindi, atakayepigiwa kura na wachezaji 20,000 duniani kote, atatangazwa tarehe 12 Januari katika tuzo la Ballon d'Or . Walioorodheshwa kwenye nafasi nyingine bado hawajatangazwa.

JESHI LA NIGERIA MDEBWEDO,HUWAKIMBIA BOKO HARAM


Viongozi wa juu wa dini ya kiislam nchini Nigeria wameli shambulia jeshi nchi hiyo na pia kuwashutumu kuwa hukimbia mashambulio yanayofanywa na kundi la kigaidi la kiislam la Boko Haram.

Bodi hiyo inayoongozwa na Sultan wa Sokoto,imesema kwamba jeshi hilo limekuwa na tabia ya kutelekeza silaha zao kwa jeshi na kukimbialia mafichoni , na pindi mambo yanapotulia hurejea uraiani na kuwatishia raia.

Maelfu ya raia wa Nigeria wamekimbilia Niger kufuatia shambulio la hivi karibuni kutoka kwa kundi hilo la Boko Haram.

Waasi hao hujifanya kuwa ni wafanyabiashara walobebelea maboksi yenye bidhaa sokoni katika mji wa Damasak mji ulio Kaskazini mwa nchi ya Nigeria.

Lakini imebainika kwamba boksi hizo huwa zimesheheni bunduki,ambazo hutumika kushambulia raia wasio na hatia.

MDOMO WAMPONZA MWANAMKE,PAKISTANI


Mwanamke mmoja amehukumiwa adhabu ya kifo nchini Pakistan kwa kosa la kufuru, naye amekwisha kukata rufaa katika mahakama kuu nchini humo,hukumu hii imekuja miaka minne nyuma baada ya kukutwa na hatia kwa kumtukana mtume Muhammad Swalalahu ale wa Salaam.

Wakiili wa Asia Bibi anaamini kwamba rufaa yao itafanikiwa na mashauri yatakuwa baada ya mwaka mmoja.

Asia anashutumiwa kwa kufuru na kikundi kimoja cha wanawake wa kiislam kwa madai ya bibi huyo kutokuwa tayari kugusa birika la maji baada ya wanawake hao kulishika kwa madai ya imani yake.

Pakistani katika sheria zake haina kawaida ya kunyonga raia wake kwa kosa la kufuru lakini mashtaka, adhabu na vifungo vimekuwepo mara kwa mara kwa makosa ya kuutusi uislam.

WAZIRI WA ULINZI WA MAREKANI,CHURK HAGEL,HAJIULIZI


Habari kutoka Pentagon zinasema kuwa, Hagel amekuwa akifanya mazungumzo na Rais Barack Obama tangu mwezi Oktoba kuhusu kujiuzulu kwake. Duru za ndani ya Pentagon zinasema Rais Obama alimuomba Hagel kujiuzulu baada ya chama chake cha Democrats kushindwa vibaya kwenye uchaguzi mdogo uliokamilika majuzi. Imedaiwa kuwa, Hagel ameshindwa kukabiliana na changamoto za hivi karibuni zinazolikabili jeshi la Marekani ikiwemo kadhia ya Afghanistan na oparesheni dhidi ya kundi la kigaidi la ISIL. Hagel ataendelea kushikilia wadhifa wake hadi papatikane shaksia mwingine wa kujaza nafasi hiyo.

Jack Reed, Seneta wa jimbo la Rhode Island ni miongoni mwa wale wanaopigiwa upatu wa kuchukua nafasi hiyo.

Sunday 23 November 2014

RADI YAUA 6 SONGEA

Watu 6 wamefariki dunia na wengine wawili kujeruhiwa wilayani Songea mkoani Ruvuma baada ya kupigwa na radi kufuati mvua kubwa iliyonyesha usiku wa kuamkia Jumamosi..

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Ruvuma ACP Mihayo Msikhela amesema kuwa maafa hayo yalitokea majira ya saa mbili usiku wakati watu hao wakila chakula cha usiku kwenye mgahawa wa chuo cha kilimo na mifugo cha Liti Madaba Songea

Kamanda huyo ameongeza kuwa mvua kubwa ilinyesha majira ya saa moja na nusu hadi saa mbili na baadaye ikapiga radi na kuua watu sita na kujeruhi watu wawili.

Amewataja waliopoteza maisha kwa kupigwa na radi kuwa ni Chesco Luoga mwanafunzi wa chuo cha Liti Madaba na mkazi wa Ludewa, Lucas Mabula mwanafunzi wa chuo hicho na mkazi wa Magu mkoani Mwanza, Eva Chapile muhudumu wa mgahawa wa chuo hicho, Osiana Antoni mhudumu wa Mgahawa wa chuo hicho, Justine Ngonyani mkulima na mkazi wa madaba Songea na Edwini Fungo mkulima na mkazi wa Madaba Songea.

Amewataja majeruhi kuwa ni Beatrice Mhagama mwanafunzi wa chuo cha Kilimo na mifugo Liti Madaba na mkazi wa Peramiho Songea na Leokadia Fusi muhudumu wa mgahawa wa chuo hicho na kwamba miili ya marehemu na majeruhi wako katika kituo cha afya Madaba.

Kutokana na tukio hilo mkuu wa mkoa wa Ruvuma Bw. Said Mwambungu na Mkuu wa wilaya ya Songea Bw.Joseph Mkirikiti wameenda eneo la tukio Madaba Songea na kueleza kusikitishwa na tukio hilo na kusema huo ni msiba mzito kwa mkoa wa Ruvuma.